Friday, April 26, 2024

WANANCHI WA SINGIDA WAMPONGEZA RAIS SAMIA KWA KUWALETEA MAENDELEO MAKUBWA.

Wananchi wa mkoa wa Singida amesherekea miaka 60 ya Muungano kwa kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuupatia mkoa wa Singida fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo imeleta mabadiliko makubwa ya kijamii.

Mkuu wa mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, akizungumza kwenye maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanzania ambayo kimkoa yamefanyika mjini Kiomboi wilayani Iramba amesema pamoja na Serikali Kuu kutoa fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo lakini bado kuna umuhimu mkubwa kwa wananchi kushirikiana na Serikali katika kujitolea nguvu kazi ili kuongeza kasi katika ukamilishaji wa miradi hiyo.

Dendego, amesema maendeleo ya kweli hayawezi kuja kama watu hawatashirikiana katika kufanya kazi hivyo ni muhimu kwa makundi yote kushirikiana kwa kiwango cha juu ili kuharakisha maendeleo yao na ya Taifa kwa ujumla.

Aidha, amewahakikishia wananchi wa mkoa huo kuwa yeye ni muumini mzuri kwa watu wanaochapa kazi kwa bidii hivyo ni lazima wananchi wote kuchapa kazi ili kujiletea maendeleo yao na ya Taifa kwa ujumla.

Katika maadhimisho hayo ya miaka 60 ya Muungano, Mkuu huyo wa mkoa ametoa zawadi mbalimbali kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika uandishi wa isha pamoja na vikundi mbalimbali vya burudani zilizotumbuiza hususan kwa wimbo maalum wa Muungano.

RC DENDEGO AKONGA NYOYO ZA WANASINGIDA KWENYE MAADHIMISHO YA MIAKA 60 YA...



Maadhimisho ya miaka 60 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yanafanyika hapa katika Wilaya ya Iramba na Kitaifa yanafanyika Dar es Salaam yakiwa na Kauli Mbiu Miaka 60 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania “Tumeshikamana na Tumeimarika, kwa Maendeleo ya Taifa letu”. 

Mkoa wa Singida unaungana na Watanzania wote katika maadhimisho haya kuanzia tarehe 14 April, 2024 hadi leo tarehe 26 April 2024 ambapo katika kipindi hicho shughuli mbalimbali zilifanyika katika Mkoa huo ikiwemo maombi na dua ya kuliombea Taifa, usafi katika maeneo ya Umma, michezo, Sanaa, utamaduni na kupanda miti kwenye maeneo mbalimbali.

Wednesday, April 24, 2024

RC DENDEGO: SEKTA YA BIASHARA NA VIWANDA NI MUHIMU KWA UCHUMI WA MKOA WA SINGIDA

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mheshimiwa Halima Dendego, amekutana na Uongozi wa Chama cha Wafanyabiashara, Wakulima na wenye Viwanda Tanzania (TCCIA) wa mkoani humo, leo Aprili 24, 2024 ofisini kwake, na kufanya nao mazungumzo yanayohusiana na sekta ya biashara ili kukuza na kuinua uchumi wa mkoa na Taifa kwa ujumla.

Kupitia kikao hicho, ujumbe wa TCCIA Mkoa wa Singida uliyoongozwa na Mwenyekiti wake Bw. Elly Kitila Mkumbo, ukiwa na lengo kwa Jumuiya hiyo ya Wafanyabiashara kujitambulisha mbele ya Mkuu huyo wa Mkoa aliyehamia Singida kutokea Mkoani Iringa hivi karibuni.

Aidha, katika kikao hicho walipata wasaa wa kujadili fursa mbalimbali kupitia Sekta ya biashara, uchumi, uzalishaji pamoja na uwekezaji zilizopo mkoani Singida hususani kwenye viwanda, kilimo, biashara, uvuvi, mifugo, madini, pamoja na miundombinu ya barabara na nishati ili ziweze kuinua na kuboresha maisha wananchi wa mkoa huo na Taifa kwa ujumla.

RC Dendego, ameuhakimishia uongozi wa Jumuiya ya Wafanyabishara hao kuwa ataimarisha ushirikiano zaidi baina ya pande zote mbili ili kukuzu uchumi wa wanasingida kupitia sekta binafsi kwakuwa Serikali ya Mkoa ipo imara katika Ulinzi na Usalama.

“Kwa kweli Jumuiya yenu ya Chamber of Commerce, ni muhimu na ni muhimili mkubwa katika uchumi, niwaombe sana tuendeleze ushirikiano huu kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wetu ambao Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuboresha maisha ya mtu mmoja mmoja ndio maana miradi mbalimbali inatekelezwa.’ amesema Dendego.

Katika mazungumzo hayo, msafara wa Jumuiya ya Chamber of Commerce, kupitia Mwenyekiti Kitila, alimweleza Dendego umuhimu wa Serikali kuboresha soko la kimataifa la vitunguu lililopo Kata ya Misuna katika Manispaa ya Singida kutokana na umuhimu wake katika kuhudumia wakulima na wafanyabishara wa ndani na nje ya Tanzania. 

Kitila amemhakikishia Mkuu huyo wa mkoa kuwa, Chamber of Commerce itaendeleza na kudumisha ushirikiano baina ya Jumuiya ya TCCIA na Serikali kwa nia thabiti ya kumkomboa na kuhakikishia mfanyabiashara shughuli zake zinatekelezeka kwa maslahi ya Taifa pamoja na kulitangaza soko la kimataifa la vitunguu lililopo mkoani Singida.

Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara, Wakulima na wenye Viwanda Tanzania (TCCIA) Mkoa wa Singida Bw. Elly Kitila Mkumbo, akizungumza kwenye kikao baina ya Mkuu wa Mkoa wa Singida na TCCIA kilichofanyika ofisini kwa Mkuu wa Mkoa huo.

Kuhusu sekta ya Mawasiliano, mmoja wa wajumbe wa Chamber of Commerce, James Japheth (Buhanzo), ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Redio Standard iliyopo Singida Mjini ameahidi kuongeza wigo wa usikivu wa Redio hiyo aliyowekeza mkoani humo ili masafa yake yaweze kupatikana kwa urahisi ndani na nje ya mkoa wa Singida.

Buhanzo alilazimika kusema hayo, baada ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, kumtaka atumie fursa ya uwekezaji wa kituo chake cha Redio kuongeza usikivu wa matangazo ili Wananchi wa mkoani humo waweze kupata habari mbalimbali za maendeleo zinazotekelezwa na Serikali pamoja na sekta binafsi.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego, akisisitiza jambo kwa Wajumbe wa kikao hicho.


Kikao kikiendelea.

Tuesday, April 23, 2024

KUELEKEA MAADHIMISHO YA MIAKA 60 YA MUUNGANO, RC SINGIDA AHIMIZA AMANI NA UTULIVU

Mkuu wa mkoa wa Singida Halima Dendego ameonya kuwa atawachukulia hatua kali watu au kikundi cha watu wanaotaka kuvuruga au kuvunja amani na utulivu kwa wananchi wa mkoa wa Singida.

Dendego, ametoa kauli hiyo (leo 23/Aprili/24 ) mjini Singida, katika uzinduzi wa wiki ya maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kufanya usafi katika maeneo mbalimbali ya Soko Kuu la Singida.

Mkuu huyo wa mkoa wa Singida amewasisitiza wananchi wa mkoa wa Singida kuwakataa watu au mtu yeyote anayetaka kumdhalilisha Rais au Watanzania kwani wakiwaruhusu kufanya hivyo watakuwa wamedhalilisha Taifa na Watanzania wote hivyo ni lazima wananchi wote waungane kukataa watu hao wenye nia mbaya na Taifa la Tanzania.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego, (wapili kushoto) akifanya usafi wa mazingira na wananchi katika soko kuu la Singida.

“Tuungane wote katika kupambana na yeyote anayetaka kuleta ujinga ujinga katika Taifa letu tuwabaini ili tuwawajibishe “ Amesisitiza Halima Dendego.

RC Dendego, amesema yeye ni rafiki wa wote Vijana, Wazee, Wanaume na Wanawake hivyo Ofisi yake ipo wazi muda wote kwa anayetaka kusaidiwa kwa shida yeyote aende ili asaidiwe nia ni kuona wananchi Singida wanaishi maisha mazuri na yenye staha bila kero.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe amemhakikishia Mkuu wa mkoa huo kuwa atasimamia maelekezo yake yote aliyotoa hasa ya kuhakikisha Manispaa ya Singida inakuwa safi katika maeneo yote ya Masoko na maeneo yenye watu wengi kama hatua ya kudhibiti magonjwa ya maambukizi ikiwemo kipindupindu.

Gondwe amesema kuwa hivi karibuni watazindua kampeni kubwa ya usafi katika Manispaa ya Singida ambayo itasaidia kuboresha usafi katika maeneo yote ya mji wa Singida ikilinganishwa na hali ilivyo sasa.

Naye, Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Edward Mboya amebainisha kuwa kupitia mapato ya ndani wanaendelea na mchakato wa kununua gari nyingine mpya ya kubebea taka na vifaa vya kuhifadhi taka lengo likiwa ni kuifanya Manispaa ya Singida kuwa bora nchini hasa katika masuala ya Usafi.

Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe, akifanya usafi wa mazingira na wananchi katika soko kuu la Singida.

Wananchi wa Singida Mjini wakifanya usafi wa mazingira ikiwa ni sehemu ya kuelekea maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Monday, April 22, 2024

MKOA WA SINGIDA WAANZA KUTOA CHANJO YA SARATANI YA MLANGO WA KIZAZI KWA WASICHANA 178,114.

Mkoa wa Singida umezindua rasmi zoezi la utoaji wa chanjo wa Saratani la mlango wa kizazi kwa wasichana mwenye umri kati ya miaka Tisa (9) hadi 14 ambapo Wasichana 178, 114 wanatarajiwa kupatiwa chanjo hiyo mkoani humo.

Akizindua zoezi la utoaji wa Chanjo hiyo katika Kijiji cha Kisaki Manispaa ya Singida, Mkuu wa mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego (leo 22-Aprili-2024 ) amewaagiza Maafisa Afya wahakikishe maeneo yote yaliyoandaliwa kutolewa huduma hiyo ya chanjo yanafanya hivyo kwa viwango vya juu ili kuwalinda watoto wa kike na saratani hiyo hatari.

Dendego amesisitiza kuwa chanjo hiyo pia ni lazima iwafikie wanafunzi wanaosoma kwenye shule binafsi na watoto wa kike ambao wanaishi mitaani nao wapate fursa ya kupata chanjo hiyo ili kuwakinga na saratari na mlango wa kizazi.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, akizungumza kwenye uzinduzi wa zoezi la utoaji wa chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi iliyofanyika kimkoa katika Shule ya Msingi Kisaki Halmashauri ya Manispaa ya Singida.

“Tunapoenda kuwalinda watoto wa kike kwa kuwachanja chanjo hiyo maana yake tunawaepusha na madhara ugonjwa wa saratani ili wasije wakaambukiza wavulana”Ameeleza RC. Halima Dendego.

Amesisitiza kuwa chanjo hiyo ni muhimu kwa wasichana na inatolewa bure kwa sababu Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa maendeleo imegharamia chanjo hiyo, hivyo ni muhimu kwa wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao kupata chanjo hiyo ili kuwaepusha na madhara yanayoweza kutokea. 

Kwaupande wake, Mganga Mkuu mkoa wa Singida Dkt. Victorina Ludovick amesema kwa Tanzania chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi (HPV) ilianza majaribio mwaka 2014 mkoani Kilimanjaro na kupata mafanikio makubwa kwa kuwakinga wasichana wasipate ugonjwa huo.

Dkt. Victorina Ludovick ameeleza mtu yeyote anaweza kuambukizwa saratani hiyo katika umri wowote ule hasa wakati wa tendo la ndoa na inaweza kusababisha magonjwa mengine ikiwemo saratani ya koo na magonjwa mengine ya via vya kizazi kwa wanamke na wanaume.

Naye, Katibu Tawala wa mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga amewataka Maafisa Afya wanaotoa chanjo hiyo kuhakikisha wanafanikisha zoezi hilo kwa viwango ili mkoa wa Singida uwe wa kwanza katika utoaji wa chanjo hiyo kwa wasichana mwenye umri wa miaka Tisa hadi 14.  

Amesema saratani hiyo inaua na ni ugonjwa hatari hivyo ni muhimu kwa watoto wote wenye umri wa kupata chanjo wapewe kutokana na umuhimu wake katika kulinda afya zao.

Nao, Mashuhuda waliopewa chanjo hiyo wakizungumza kwenye uzinduzi wa utoaji wa chanjo ya satarani la mlango wa kizazi katika kijiji cha Kisaki Manispaa ya Singida Lukuresia Andrea na Salisabila Athumani wote wakazi wa mkoa wa Singida wamesema tangu wapatiwe chanjo hiyo hawajapata madhara yoyote hivyo wameomba wazazi na walezi wasiwazuie watoto wao wa kike kwenda kupata chanjo hiyo kwa sababu inafaida kubwa katika maisha yao.


Katibu Tawala wa mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga akizungumza kwenye uzinduzi wa zoezi la utoaji wa chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi.

Zoezi la kuimarisha chanjo ya HPV litakamilika tarehe 26 Aprili, 2024 hata hivyo hudumaa hiyo itaendelea kutolewa kwa utaratibu wa zamani yaani shuleni, vituo vya kutolea huduma za afya na kwenye huduma za mkoba za Masuala ya Afya ya Uzazi na Mtoto.

Chanjo ya HPV, kama ilivyo kwa chanjo nyingine zinazotolewa kupitia Mpango wa Taifa wa Chanjo, haiuzwi kwa mteja yeyote, hivyo inatolewa bure kwa walengwa katika vituo vyetu vya kutolea huduma.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego (mwenye koti rangi nyekundu), akiwa na wanawake waliopata chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi mkoani Singida waliokaa na watoto wao, Pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali.

Baadhi ya Wanawake waliopata chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi mkoani Singida wakiwa na watoto wao.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida Victorina Ludovick, akisoma taarifa ya utoaji wa chanjo katika Mkoa huo.

Wanafunzi kutoka Shule mbalimbali waliohudhuria kushuhudia na kupata huduma wakati wa zoezi la uzinduzi utoaji wa chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi katika kijiji cha Kisaki Manispaa ya Singida.