Tuesday, November 18, 2025

RC DENDEGO ASISITIZA UBUNIFU KATIKA UANDAAJI WA TAKWIMU

 

.                           

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ameongoza kikao cha Maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika 2025 kwa ngazi ya kanda kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida Novemba 18,2025, Kikao  kilichowakutanisha wadau kutoka mikoa ya Manyara, Morogoro, Dodoma na Singida kwa lengo la kujadili umuhimu wa takwimu katika kuimarisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi. 

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Dendego alisema matumizi ya takwimu sahihi ni nyenzo muhimu ya kupanga na kutekeleza mipango ya maendeleo, hasa katika kipindi ambacho dunia inapitia mageuzi ya teknolojia.


Amesisitiza kuwa ni muhimu wadau wote wakiwemo serikali, sekta binafsi na taasisi za kiraia kuongeza ubunifu katika ukusanyaji na matumizi ya takwimu ili kuhakikisha maamuzi yanayofanyika yanakuwa na tija kwa jamii. Aidha, alitoa pongezi kwa waandaaji wa maadhimisho hayo kwa kulipa uzito kundi la wanahabari, akieleza kuwa vyombo vya habari vina mchango mkubwa katika kufikisha taarifa sahihi kwa umma na mara nyingi hutumia takwimu kama msingi wa habari zao.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Meneja wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Mkoa wa Singida, Bw.Naing'oya Kipuyo, alisema takwimu ni nguzo muhimu katika maendeleo ya taifa kwa kuwa zinawezesha serikali na wadau kupanga miradi kwa kuzingatia mahitaji halisi ya wananchi. Alieleza kuwa takwimu sahihi huimarisha uwajibikaji na utawala bora, kwani viongozi wanawaletea wananchi taarifa za uhakika kuhusu rasilimali na huduma za kijamii. Aidha, alibainisha kuwa takwimu hutumiwa na wawekezaji kutambua fursa za kiuchumi na kufanya maamuzi sahihi, jambo linalochochea ukuaji wa uchumi na kujenga mazingira bora ya biashara.

Bw. Kipuyo aliongeza kuwa takwimu rasmi husaidia kudhibiti upotoshaji wa taarifa na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu hali ya sekta mbalimbali kama elimu, afya na ajira. Alifafanua kuwa takwimu ndizo msingi wa kutathmini utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), hivyo kusaidia taifa kutambua maeneo yanayohitaji maboresho. Aidha, alisema mchakato wa ukusanyaji na uchambuzi wa takwimu unachochea matumizi ya teknolojia na ubunifu katika taasisi za umma na binafsi, na hivyo kuwezesha maamuzi yenye tija yanayochangia maendeleo ya jamii kwa ujumla.

Miongoni mwa watoa mada katika maadhimisho hayo alikuwa Mwandishi wa Habari wa Gazeti la Nipashe mkoa wa Singida, Thobias Mwanakatwe. Katika mada yake, Mwanakatwe alieleza kuwa matumizi sahihi ya takwimu rasmi na vyombo vya habari ni nguzo muhimu katika kujenga jamii inayojali haki, amani na maendeleo. Alisema takwimu zinapowasilishwa kwa umma kwa usahihi na uwazi husaidia wananchi kuelewa hali halisi ya sekta mbalimbali kama elimu, afya, uchumi na huduma za kijamii.

Aidha, Mwanakatwe alibainisha kuwa takwimu rasmi zinapochambuliwa na kuripotiwa vyema na vyombo vya habari husaidia kuzuia upotoshaji, kuimarisha uwajibikaji wa viongozi na kufanya maamuzi yenye tija kwa jamii. Alisisitiza kuwa vyombo vya habari vinapozingatia ukweli wa takwimu vinakuwa sehemu ya suluhisho la changamoto za kijamii badala ya kuwa chanzo cha migogoro au upotoshaji. Pia aliongeza kuwa uandishi wa habari unaotumia takwimu rasmi huibua maeneo yanayohitaji maboresho na kuimarisha misingi ya utawala bora.

Kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ni “Kuongeza ubunifu katika matumizi ya takwimu na taarifa ili kujenga jamii jumuishi inayojali haki, amani na maendeleo kwa Waafrika.” Kaulimbiu hii inalenga kusisitiza umuhimu wa matumizi bunifu ya takwimu katika kuimarisha utawala bora na ustawi wa jamii.








Thursday, November 13, 2025

SINGIDA YAWEKA MIKAKATI KUMALIZA VIFO VYA MAMA NA MTOTO

 

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewataka viongozi wa sekta ya afya kuhakikisha wanapunguza idadi ya vifo vitokanavyo na uzazi na vifo vya watoto wachanga, akisisitiza umuhimu wa kutumia ipasavyo rasilimali zilizotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Ametoa maagizo hayo katika kikao cha kujadili mwenendo wa vifo vya kina mama na watoto wachanga kwa robo ya Julai hadi Septemba 2025 kilichofanyika katika ukumbi wa ofisi ya Halmashauri ya Manispaa ya Singida, ambapo amewataka wakurugenzi wa halmashauri na waganga wakuu wa wilaya kuongeza uwajibikaji na ubunifu katika kuboresha huduma za afya.

Dkt. Mganga amesema Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya afya kupitia ujenzi wa miundombinu, usambazaji wa vifaa tiba, na kuongeza bajeti ya dawa, hivyo viongozi wa afya wanapaswa kuhakikisha rasilimali hizo zinatumika kwa tija ili kuokoa maisha ya wananchi. “Serikali imeleta miundombinu na vifaa kwa ajili ya Watanzania wote, hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha tunavitumia kupunguza vifo vya kina mama na watoto,” amesema.

Akiendelea kutoa maagizo, Dkt. Fatuma amewataka waganga wakuu na wakurugenzi kutoa elimu kwa wanawake na wanaume hata kabla ya kupata ujauzito, ili kujenga uelewa wa pamoja kuhusu afya ya uzazi na kuzuia vifo vinavyotokana na kukosa elimu. “Tusichague hadhira ya kuielimisha, watu sahihi si wale wanaokuja hospitalini wakiwa wajawazito tayari. Tuelimishe jamii nzima wajue namna ya kujiandaa na kutunza ujauzito wenye afya bora,” amesema.

Pia amezitaka kamati zote zinazohusiana na ufuatiliaji wa vifo vya kina mama na watoto wachanga kuimarishwa, huku akiwasihi wananchi kutumia vituo vya afya vilivyo karibu wakati wa dharura badala ya kusafiri umbali mrefu, ili kuokoa maisha ambayo yangepotea kwa kuchelewa kupata huduma.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Victorina Ludovick, amesema kuwa wakina mama  hupoteza maisha kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo kutokwa na damu nyingi na matatizo ya upumuaji kwa watoto wachanga. Amesema uongozi wa afya umeongeza jitihada katika kuhakikisha dawa zinapatikana, huduma za rufaa zinaboreshwa, na magari ya wagonjwa yanakuwa tayari muda wote kwa ushirikiano na madereva jamii.

Viongozi wa hospitali na waganga wakuu wa halmashauri zote za Singida wameahidi kuendelea kushirikiana katika kutoa elimu, kuongeza uwajibikaji na kutumia kwa ufanisi rasilimali zilizotolewa na Serikali ili kuhakikisha vifo vya kina mama na watoto wachanga vinapungua kwa kiwango kikubwa.




Tuesday, November 11, 2025

WATUMISHI WAAGIZWA MATOKEO CHANYA YA FEDHA ZA SERIKALI

 


Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Daktari Fatuma Mganga, amewaagiza Wakuu wa Sehemu, Idara na Vitengo kuhakikisha wanazalisha matokeo mazuri na chanya kutokana na fedha zinazotolewa na Serikali, sambamba na kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana katika miradi inayotekelezwa.

Daktari Mganga alitoa maagizo hayo leo wakati wa kikao cha Kamati ya Bajeti cha robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/2026 kilichofanyika katika ofisi za Sekretarieti ya Mkoa wa Singida.

Amesema ni muhimu kwa viongozi kuhakikisha fedha zinazotolewa zinatumika kwa ufanisi na kuleta tija kwa wananchi, sambamba na ufuatiliaji wa karibu wa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Katika kikao hicho, wajumbe walijadili masuala mbalimbali yakiwemo taarifa za utekelezaji wa bajeti, mpango wa matumizi ya fedha, pamoja na changamoto za utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika mkoa huo.

Aidha, Katibu Tawala ametoa pongezi kwa vitengo vya Sheria, Ugavi na Ununuzi, Miundombinu na Uhasibu kwa ushirikiano mkubwa waliouonyesha na kufanikisha miradi kadhaa kukamilika kwa ubora wa hali ya juu.

Akihimiza uwajibikaji, Dkt. Mganga aliwataka viongozi wote kuwasimamia watumishi waliopo chini yao katika kujaza ipasavyo mfumo wa upimaji wa utendaji kazi wa watumishi (PEPMIS) kulingana na majukumu wanayoyatekeleza. Pia aliagiza kila kiongozi kutambua viashiria vya utendaji vinavyopima mafanikio ya idara yake ili kuhakikisha utekelezaji bora wa majukumu yao.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Wakuu wa Idara na Vitengo, pamoja na Makatibu Tawala wa Wilaya za mkoa wa Singida. Kikao hicho kiliendeshwa na Katibu Tawala wa Mkoa, huku Katibu wa kikao hicho akiwa Bw. Nesphory Bwana, Katibu Tawala Msaidizi – Sehemu ya Mipango na Uratibu.






 


Monday, October 27, 2025

SERIKALI YAMWAGA MABILIONI UJENZI WA OFISI NA NYUMBA ZA MAKAZI SINGIDA


Sekretarieti ya Mkoa wa Singida imepokea zaidi ya shilingi bilioni tatu kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya ujenzi wa majengo mbalimbali ya viongozi wa serikali mkoani humo.

Fedha hizo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa serikali wa kuboresha miundombinu ya ofisi na makazi ya viongozi katika ngazi za mikoa na wilaya. Kupitia mpango huo, ofisi tatu za wakuu wa wilaya zitajengwa katika Wilaya za Iramba, Manyoni na Singida, ambapo kila moja imetengewa bajeti ya shilingi bilioni moja (1,000,000,000).

Aidha, serikali imetenga kiasi cha takribani shilingi milioni 454 kwa kila nyumba ya makazi ya Wakuu wa Wilaya za Manyoni na Iramba, sambamba na bajeti ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida.

Akizungumza leo Oktoba 27, 2025, wakati wa ziara yake katika Wilaya ya Iramba, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego amefika katika eneo lililopendekezwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi mpya ya Mkuu wa Wilaya ya Iramba na nyumba ya makazi ya Mkuu wa Wilaya hiyo, ambapo alijadiliana na viongozi wa eneo hilo kuhusu maandalizi ya utekelezaji wa mradi huo.

Kupatikana kwa majengo hayo mapya kutaboresha kwa kiasi kikubwa mazingira ya kazi na utendaji wa viongozi wa serikali, kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi, pamoja na kuimarisha usimamizi wa shughuli za maendeleo katika wilaya na mkoa kwa ujumla. 

Vilevile, ujenzi huo utachochea fursa za ajira za muda mfupi kwa wananchi wa maeneo husika na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Singida.









 


Saturday, October 25, 2025

RC DENDEGO ATETA NA WATUMISHI USHIRIKI UCHAGUZI


 Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ameongoza kikao na wakuu wa taasisi pamoja na watumishi wote wa Serikali wa Mkoa wa Singida leo, Oktoba 25, 2025, chenye lengo la kuwahamasisha kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano ijayo, Oktoba 29, 2025.


Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Dendego amewakumbusha watumishi na wakuu wa taasisi kuzingatia maelekezo ya kisera yaliyotolewa kuelekea Uchaguzi Mkuu, 

Akiwakumbusha maelekezo yake ya kisera kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewataka watumishi wote wa umma kuhakikisha wanakuwa na vitambulisho halali vya wapigakura na kufika mapema katika vituo vyao vya kupigia kura kabla ya muda wa kufungwa. Amesisitiza kuwa watumishi wanapaswa kuwa mfano wa utii kwa sheria kwa kufuata kikamilifu maelekezo ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) pamoja na viongozi wa usalama, ili kuhakikisha mchakato mzima wa uchaguzi unafanyika kwa amani, utulivu na uwazi.

Aidha, amekemea vikali vitendo vinavyoweza kuashiria upendeleo wa kisiasa, akiwataka watumishi kuepuka kuvaa mavazi au kubeba nembo za vyama vya siasa, pamoja na kujiepusha na matamshi, maandiko au mienendo yoyote inayoweza kuchochea chuki, vurugu au ubaguzi katika jamii. Ameongeza kuwa watumishi wanapaswa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na uwajibikaji, bila kuegemea upande wowote wa kisiasa, ili kudumisha heshima ya utumishi wa umma na kuonesha mfano bora wa uadilifu katika kipindi chote cha uchaguzi.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewataka watumishi wote kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii, hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi, na badala yake kutumia mitandao hiyo kwa elimu, uhamasishaji chanya na kuimarisha umoja wa kitaifa.

Aidha, Dkt. Mganga ametoa wito wa kujilinda binafsi na kulinda familia, kwa kuepuka kutembea katika maeneo hatarishi hasa nyakati za usiku, na kufanya majukumu yao mapema ili kuepuka usumbufu wowote siku za uchaguzi.

Nao wakuu wa taasisi mbalimbali mkoani Singida, wameahidi kujitokeza mapema ifikapo saa moja asubuhi siku ya uchaguzi, kuhakikisha wanatekeleza haki yao ya kikatiba ya kupiga kura, na kuwa mfano bora kwa watumishi na wananchi kwa ujumla.








Monday, October 20, 2025

SOKO JIPYA LA VITUNGUU,WAFANYABIASHARA KUPINDUA MEZA KIUCHUMI


 Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ameagiza viongozi wa Halmashauri kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wakandarasi wanaotekeleza ujenzi wa Soko jipya la Vitunguu lililopo Kititimo, ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati uliopangwa na kwa viwango vya juu.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika eneo jipya la ujenzi wa soko hilo, Mhe. Dendego amesema Serikali ina dhamira njema ya kuboresha mazingira ya wafanyabiashara na kuhakikisha Singida inakuwa kitovu cha biashara ya vitunguu nchini.

“Singida tunakwenda kipindua meza, tunakwenda kuweka historia ya kipekee kwa mradi huu mkubwa na wa kipekee. Hii ni moja ya sababu ya kwenda kuuweka mkoa wa Singida kwenye ramani ya kuwa Jiji la Singida. Na hili linawezekana kwa utekelezaji wa miradi hii mikubwa. Tutegemee mwezi Septemba 2026 kukata keki ya mafanikio baada ya kukamilika kwa mradi huu wa TACTIC,” amesema Mhe. Dendego.

Kadhalika, amemtaka mkandarasi kuhakikisha maeneo muhimu yanazingatiwa katika ujenzi wa soko hilo ikiwemo maeneo ya zahanati, michezo, mapumziko, kumbi za mikutano pamoja na maeneo ya sekta binafsi kuwekeza katika huduma za kifedha. Amesisitiza pia kazi kufanyika kwa ubora ili gharama kubwa za ujenzi ziendane na thamani ya fedha zilizotolewa na Serikali.

Awali, Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, aliwataka wajumbe wa kikao hicho kufikisha salamu za Serikali kwa wananchi na wafanyabiashara wa Soko la Vitunguu juu ya nia njema ya kuhamishia soko hilo maeneo mapya. Amesema eneo hilo jipya litakuwa rafiki zaidi kwa wafanyabiashara na litakidhi idadi kubwa ya wajasiriamali kuliko soko la sasa, hivyo kuongeza faida maradufu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Soko la Vitunguu-Misuna, Bw. Iddi Mwanja, amesema wafanyabiashara wamepokea kwa mikono miwili na kwa furaha kubwa mradi wa soko jipya kwa kuwa utawanufaisha kwa kiasi kikubwa sambamba na kufanya kazi zao kwa uhuru katika mazingira bora na rafiki kwa wote.

“Serikali yetu tunaiamini, tuiache ifanye kazi yake. Tutafuata utaratibu tunaopewa kwa sababu ina nia njema kwetu sisi wananchi,” amesema Bw. Mwanja.

Naye Katibu wa Soko la Vitunguu, Bw. Mshujaa Salum Mwacha, amesema hawana hofu kwani viongozi wamekuwa wakiwasikiliza na kuwashirikisha vizuri katika kila hatua ya maandalizi ya mradi huo. Ameongeza kuwa wamefurahia kuona soko jipya limewapa kipaumbele watu wenye mahitaji maalum sambamba na akinamama wanaonyonyesha.

Mkandarasi anayehusika na ujenzi huo ameahidi kuhakikisha ujenzi unakuwa wa viwango vya juu na unakamilika kwa wakati, akisisitiza kuwa wananchi wa Singida wajiandae kupokea soko zuri la kisasa lenye mazingira rafiki kwa kazi zao za kila siku.Amesema kuwa ukubwa wa soko hilo ni mita za mraba 32,547.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Katibu Tawala wa Wilaya, Wajumbe wa Soko la Vitunguu, Afisa Mazingira, Afisa Maendeleo ya Jamii, Mtaalam wa Ardhi, wataalam kutoka TARURA, wakandarasi na wadau wengine wa maendeleo.

Mradi huu wa ujenzi wa Soko jipya la Vitunguu unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya biashara mkoani Singida kwa kuboresha mazingira ya wafanyabiashara, kuongeza mapato ya Serikali, kutoa ajira kwa wananchi, pamoja na kuongeza thamani ya zao la vitunguu linalolimwa kwa wingi katika mkoa huo. Soko hilo pia litakuwa na miundombinu rafiki kwa watu wote, likiwa na huduma muhimu kama zahanati, maeneo ya mapumziko, michezo na huduma za kifedha, hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Singida na kuchangia utekelezaji wa mpango wa kuifanya Singida kuwa Jiji la kisasa.