Saturday, June 21, 2025

NDOTO YA SINGIDA KUWA KITUO CHA VIWANDA VYA KISASA TANZANIA KUTIM


Posted on: June 21st, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego amesema kuwa Mkoa wa Singida umejipambanua kuwa kitovu cha viwanda vya kisasa nchini kupitia juhudi mbalimbali za kuboresha mazingira ya biashara, uwekezaji, na matumizi ya rasilimali zilizopo kikamilifu. 

Akizungumza katika Mkutano wa Baraza la Biashara la Mkoa wa Singida uliofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mhe. Dendego amesema kuwa Mkoa wa Singida umeendelea kuongeza idadi ya viwanda hadi kufikia 1,565 huku akibainisha kuwa viwanda vikubwa vimefikia 9, vya kati 11, vidogo 420 na vidogo sana 1,225 ambavyo kwa pamoja vinazalisha ajira kwa vijana na kuongeza mzunguko wa fedha kwa wananchi.

Amesema maendeleo haya ni matokeo ya mazingira bora yaliyowekwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha Tanzania inaingia katika uchumi wa viwanda kupitia uwekezaji wenye tija unaolenga kutumia rasilimali zinazopatikana katika kila mkoa. Ameongeza kuwa Mkoa wa Singida una rasilimali nyingi zikiwemo kilimo, madini, mifugo, na eneo zuri la kijiografia ambalo linaifanya Singida kuwa sehemu bora ya uwekezaji nchini.

Katika kuhakikisha kuwa viwanda hivyo vinaendelea kuzalisha kwa ufanisi, Mhe. Dendego amesema Serikali ya Mkoa imeweka mkazo mkubwa kwenye kilimo cha kisasa ambacho kinazalisha malighafi kwa ajili ya viwanda vya usindikaji. Aidha, amesema Mkoa unatarajia kuanza ujenzi wa soko la kimataifa la vitunguu kupitia mradi wa TACTIC kwa mwaka wa fedha 2025/2026, ambapo tayari mikataba imeshasainiwa.

 “Hii ni hatua kubwa ambayo itawainua wakulima wetu kwa kuwapatia soko la uhakika na kuongeza kipato chao kupitia thamani ya mazao wanayoyazalisha,” amesema Mhe.Dendego.

Kadhalika,ameongeza kuwa Serikali ya Mkoa inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa kushirikiana na taasisi kama TANESCO, TARURA, SUASA, na TANROADS katika kuhakikisha huduma za msingi kama umeme, maji, na barabara zinapatikana kwa urahisi katika maeneo yote ya Mkoa wa Singida. Amesema kuwa pamoja na fursa za kilimo, Mkoa pia una fursa kubwa katika sekta ya madini ikiwemo dhahabu, gypsum, shaba, aluminium na shaba nyeusi, na kwamba wawekezaji wanakaribishwa kuwekeza kwa wingi katika maeneo haya.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, akihitimisha mkutano huo, amewapongeza wajumbe wote kwa michango yao chanya iliyolenga kukuza uchumi wa mkoa. Amesema kikao hicho ni muhimu kwa kuwa uwekezaji na biashara ndiyo njia pekee ya kuzalisha fedha, siyo ajira pekee. Amewataka watumishi wa umma katika halmashauri kuwa na uelewa wa mazingira ya biashara ili kushirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kutengeneza mazingira rafiki ya uwekezaji.

 Dkt. Mganga amesema kuwa kikao hicho cha Baraza la Biashara kina umuhimu mkubwa kwa kuwa kinatoa majadiliano yatakayoleta maboresho ya mazingira ya biashara na uwekezaji akisema ni lazima taasisi za umma zichukue nafasi yake katika kuweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi ili kushirikiana katika uchumi. 

"Tukisikia tajiri mkubwa duniani hana ajira ya kawaida, wote ni wafanyabiashara. Biashara ndiyo njia pekee ya kuzalisha fedha. Wananchi wakizalisha fedha na sekta binafsi ikiongezeka, basi mzunguko wa fedha utaongezeka na ustawi wa jamii utaonekana," amesema.

Dkt. Mganga amesema mkoa umeweka kipaumbele katika kuhakikisha kuwa wakulima wanajiunga na vyama vya ushirika ili waweze kupata tija zaidi kwenye uzalishaji wao. Aidha, amepongeza juhudi za wakurugenzi wa halmashauri kwa kuboresha miundombinu na kuwafanya wawekezaji kuwa na mazingira rafiki ya kuwekeza huku akisisitiza kila halmashauri kutekeleza mpango wa kuwa na One Business Center ili wananchi wapate elimu ya biashara na uwekezaji kwa ukaribu zaidi.

Naye Katibu Tawala Msaidizi sehemu  ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Bi. Donatila Vedasto ametoa taarifa ya hali ya biashara na uwekezaji katika Mkoa akisema kuwa Mkoa wa Singida una fursa nyingi sana ambazo zinahitaji kushirikiana kati ya sekta ya umma na sekta binafsi ili kuziwezesha kutumika ipasavyo.

 Amesema kuwa mpaka sasa kuna wafanyabiashara waliopo na wanaolipa kodi wapatao 10,400 waliopo kwenye makundi ya wakubwa, wa kati, na wadogo, huku machinga walioandikishwa ni 15,898. Amesema hatua hiyo inaonesha mwelekeo mzuri wa utayari wa wananchi kuingia kwenye sekta ya biashara.

Ameongeza kuwa sekta ya uwekezaji inahitaji msukumo zaidi kutoka kwa wawekezaji wa ndani hususan kwenye maeneo ya huduma kama Shopping Malls, Resting Places, na vitega uchumi vya halmashauri ili kuongeza mapato akibainisha kuwa Mkoa wa Singida umejipambanua kama mkoa tajiri wenye rasilimali nyingi za kuendeleza viwanda na biashara zenye tija kubwa kwa Taifa.

Wajumbe wa Baraza la Biashara wakiwemo kutoka sekta za madini, TRA, OSHA, COPRA na taasisi nyingine wameelezea namna Mkoa wa Singida unavyotoa fursa adhimu kupitia madini mbalimbali kama dhahabu, gypsum, aluminium, chumvi na shaba. Pia wamependekeza kuanzishwa kwa majukwaa ya pamoja baina ya wadau wa sekta binafsi na umma ili kusikiliza changamoto na kutoa mapendekezo ya pamoja yatakayowezesha maendeleo ya haraka ya sekta ya biashara.

Kikao cha Baraza la Biashara Mkoa wa Singida pia kimehimiza kuangalia upya namna bora ya kuwawezesha wakulima kupitia vyama vya ushirika ili kuondokana na dhuluma za bei na kupatikana kwa malighafi ya kutosha kwa viwanda. Aidha, kikao hicho kimeazimia kuwepo kwa ushirikiano zaidi kati ya taasisi za serikali na sekta binafsi ili kuhakikisha Mkoa wa Singida unafikia azma ya kuwa kitovu cha viwanda vya kisasa nchini.



Tuesday, June 17, 2025

RC DENDEGO: “MKURUGENZI BANANA NA WANAOZALISHA HOJA MPYA – TUNATAKA KUWAWAJIBISHA KWA MATOKEO”.

 

Posted on: June 17th, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, akiwa mgeni rasmi katika mikutano maalum ya Baraza la Madiwani kwa Halmashauri za Wilaya ya Ikungi na Mkalama, ametoa maagizo ya moja kwa moja kwa Wakurugenzi na Watendaji wote kuhakikisha hoja zote za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zinafungwa ifikapo Julai 15, 2025, huku akipiga marufuku kuzalisha hoja mpya kwa kisingizio chochote akionya kuwa hoja mpya ni dalili ya uzembe wa moja kwa moja na ni hatari kwa ufanisi wa Serikali.

RC Dendego amesisitiza kuwa hayuko tayari kuona hoja mpya zikizaliwa kwa sababu hiyo ni sawa na kuruhusu maradhi katika mfumo wa utendaji kazi wa Serikali. 

"Kwa hiyo Mkurugenzi, banana na yeyote anayezalisha hoja mpya. Tukiona hoja mpya, tunajua kuna mtu anakula bila kunawa. Huo ni uzembe, na uzembe ni kipindupindu kwenye ofisi yako,” amesema kwa lugha ya picha akiwataka viongozi wa halmashauri kuhakikisha uwajibikaji wa hali ya juu.

Kadhalika,ameelekeza kuwa kabla ya Uchaguzi Mkuu, kila uamuzi wa Baraza la Madiwani uliofikiwa kabla ya kuvunjwa kwa mabaraza utekelezwe kikamilifu akisisitiza kuwa utekelezaji wa maamuzi ya mabaraza ni sehemu ya heshima kwa madiwani waliomaliza muda wao, na ni msingi wa kuendeleza imani kwa wananchi.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amesema kuwa ufuatiliaji wa hoja za ukaguzi lazima ufanyike kwa maandishi na kwa nyaraka zenye ushahidi wa hatua zilizochukuliwa. 

Ameongeza kuwa Halmashauri hazipaswi kutegemea vyanzo vya kawaida pekee katika mapato, bali ziendelee kubuni miradi ya kimkakati kama vile uwekezaji wa hewa ya ukaa na uanzishaji wa viwanda vidogo ili kuongeza mapato endelevu.

Aidha, Dkt. Mganga aliwakumbusha wakurugenzi na wataalamu kuwa uandaaji wa taarifa, matumizi sahihi ya mifumo ya kielektroniki na utunzaji wa kumbukumbu ni msingi wa uwajibikaji akihimiza  Halmashauri kubuni vyanzo vipya vya mapato ikiwemo uwekezaji wa hewa ya ukaa, ujenzi wa viwanda vidogo na kuimarisha usimamizi wa rasilimali ardhi na mazao ya kilimo.

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mkoa wa Singida, Bw. Othman Mwinjuma Jumbe, ameeleza kuwa kwa Halmashauri ya Mkalama, hoja nyingi zimepatiwa ufumbuzi lakini bado kuna hitaji kubwa la kuimarisha elimu kwa watendaji kuhusu namna ya kuandaa nyaraka, kufunga hoja na kuepuka hoja mpya. Kadhalika ameunga mkono hatua zinazochukuliwa na kuahidi ushirikiano wa karibu na kila halmashauri katika kusafisha na kuimarisha mifumo ya udhibiti wa fedha.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Mhe. Thomas Apson, amebainisha kuwa Halmashauri yake imekusanya mapato kwa zaidi ya asilimia 140 ya lengo na wameweka mikakati ya kubaini mianya ya upotevu wa mapato, hususani kwenye sekta ya kilimo na biashara huku akiahidi kuongeza msukumo katika utekelezaji wa maelekezo ya RC kwa kushirikiana na wataalamu waliopo katika kila kata.

Kadhalika Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Mhe. Moses Machali, amesema kuwa nidhamu ya fedha, matumizi sahihi ya sheria na usimamizi wa hoja kwa wakati ndio silaha pekee ya kulinda maendeleo ya wananchi akisisitiza kuwa Serikali haitavumilia ulegevu wowote kutoka kwa watendaji wa ngazi yoyote ile.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Ikungi, Mh. Ally Juma Mwanga, alisema kuwa kati ya hoja 26 za ukaguzi, saba zimefungwa na 19 bado ziko kwenye mchakato wa utekelezaji. Alimhakikishia Mkuu wa Mkoa kuwa wataendelea kusimamia utekelezaji wa maamuzi na hoja kwa karibu na kwa kasi inayotakiwa ili kufanikisha maelekezo ya Serikali.

Kadhalika,Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mkalama  Mhe. James Mkwega alitoa pongezi kwa uongozi wa Mkoa kwa usimamizi madhubuti wa miradi ya maendeleo na kupendekeza kuwa uwanja wa Bombadia ubatizwe jina la Dendego, akisema Mkuu huyo wa Mkoa amekuwa mfano wa kiongozi anayetenda kwa vitendo katika kuhamasisha utekelezaji wa miradi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ikungi, Bw. Kastory Msigala, amesema kuwa hoja zote zipo katika hatua nzuri za utekelezaji, na akatoa wito kwa Wakuu wa Idara kuhakikisha hawasubiri kukumbushwa bali wachukue hatua kwa wakati. Kadhalika ameahidi kuwa ofisi yake itafikia lengo la kufunga hoja zote ndani ya muda uliowekwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mkalama, Bi. Asia Messos, alisema kuwa Halmashauri hiyo imeendelea kupokea hati safi kwa miaka minne mfululizo na sasa inahakikisha hoja zote zilizopo zimefungwa kupitia njia za maridhiano, ushauri wa kitaalamu na ufuatiliaji wa karibu.

Mikutano hiyo maalum ya baraza la madiwani imefanyika ikiwa ni sehemu ya hatua za mwisho kabla ya kuvunjwa kwa mabaraza yote nchini kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi mkuu wa serikali za mitaa. Mkoa wa Singida umeonesha dhamira ya kweli ya kuhakikisha kila hoja ya ukaguzi inashughulikiwa kwa matokeo, si kwa maneno pekee bali kwa ajili ya wananchi.

Kwa ujumla Mikutano hiyo maalum ya mabaraza maalum imefanyika kwa mafanikio makubwa kabla ya kuvunjwa kwa mabaraza ya madiwani nchini kote, ikiwa ni agizo kutoka Ofisi ya Rais – TAMISEMI. Mkoa wa Singida, chini ya uongozi wa Mkuu wa Mkoa Mhe. Halima Dendego, umeonesha msimamo thabiti wa kuhakikisha hoja za ukaguzi hazibaki kama historia, bali zinapatiwa majibu na hatua, huku fedha za umma zikisimamiwa kwa tija na ufanisi kwa maendeleo ya wananchi.

Monday, June 16, 2025

HALMASHAURI ZAAGIZWA KUFANYA KAZI KWA WELEDI ILI KUFUTA HOJA ZA CAG

 

Posted on: June 16th, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametoa maagizo kwa viongozi na watendaji wa halmashauri za Wilaya ya Itigi na Manyoni kuhakikisha kuwa hoja zote za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zinazotokana na mapungufu ya ndani zinatekelezwa kwa weledi na kufutwa kabisa. 

Akizungumza katika vikao maalum vya mabaraza ya madiwani vya kupitia taarifa ya utekelezaji wa hoja za ukaguzi kwa mwaka wa fedha, Mhe. Dendego alisema kuwa ni aibu kwa halmashauri kuendelea kuwa na hoja zinazoweza kuzuilika kwa nidhamu na uwajibikaji wa ndani. Alieleza kuwa hatua kubwa ya mabadiliko inaonekana, hasa kwa Halmashauri ya Itigi iliyopunguza hoja kutoka 40 hadi 11, akisisitiza kuwa juhudi hizo ziimarishwe zaidi hadi kufikia hoja sifuri. 

Kadhalika ameipongeza Itigi kwa kiwango kizuri cha ukusanyaji mapato ya asilimia 98.7 na kuelekeza kifikie asilimia 100, sambamba na kuhakikisha fedha za lishe na asilimia 10 kwa wanawake zinatumika kwa wakati na ufanisi. Aidha, alitoa maagizo kwa halmashauri zote kukata mishahara ya watumishi waliokopeshwa na hawajarejesha, huku akielekeza kuwa fedha zote za miradi ya maendeleo ziheshimiwe na kutumika kikamilifu ndani ya mwaka wa fedha. 

Mhe. Dendego pia amewataka madiwani kuhakikisha wanasimamia kikamilifu matumizi ya rasilimali na miradi ya wananchi, huku akiwataka watendaji kuhakikisha mifumo ya ndani ya usimamizi wa fedha inaimarika na kuwa endelevu akisisitiza kuwa lengo la Mkoa wa Singida ni kuwa na halmashauri zenye hoja chache au sifuri, jambo linalowezekana kwa mshikamano kati ya watendaji na viongozi wa kisiasa.

Akizungumza katika kikao hicho,Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amesema kuwa Itigi imefanya vizuri katika kushughulikia hoja na kwamba hatua hiyo ni mfano kwa halmashauri nyingine huku akisisitiza umuhimu wa kujaza mfumo wa PEPMIS kwa wakati ili watumishi stahiki wapate fursa za kupandishwa vyeo kwa haki. 

Kadhalika amehimiza Halmashauri kuangalia fursa mpya za kiuchumi kwa kuanzisha kampuni maalum (SPV) itakayowezesha halmashauri kunufaika na mapato mapya kupitia miradi rafiki kwa mazingira kama vile biashara ya hewa ya ukaa. Dkt. Mganga alisema kuwa mabadiliko ya kimfumo ni lazima yasimamiwe kisera lakini pia kwa ubunifu wa ndani katika vyanzo vya mapato visivyo tegemezi.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, Mhe. Hussein I. Simba, amesema kuwa mwelekeo ulioasisiwa na Mkuu wa Mkoa umeifanya halmashauri kuwa makini katika usimamizi wa hoja na kutumia vikao vya kisekta na kamati za ndani kufuatilia kila hoja hadi kufikia utekelezaji wake.

                       Amesema kuwa dhamira ya halmashauri ni kufuta kabisa hoja zote kabla ya ukaguzi unaofuata.

 Naye Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Ayoub Juma Kambi, alisema kuwa ushirikiano wa karibu kati ya ofisi yake na madiwani umechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza hoja na kutekeleza maagizo yote ya ukaguzi. Alibainisha kuwa fedha za lishe zilitumika kikamilifu na kuwa asilimia 10 kwa wanawake zimeshapokelewa na vikundi husika kwa matumizi ya maendeleo.

Katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Mkuu wa Mkoa aliwataka madiwani na watendaji kuendeleza nidhamu ya ufuatiliaji wa hoja, huku akipongeza hatua ya halmashauri hiyo kupata hati safi. Alielekeza kuwa ni wakati sasa wa Manyoni kuongoza kwa kuzuia kabisa hoja mpya kupitia mifumo thabiti ya usimamizi. 

Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Mhe. Jumanne Shabani Mlagaza, alisema kuwa halmashauri yake imejipanga kuhakikisha hoja zote zilizobaki zinapewa kipaumbele na kutatuliwa kwa wakati akisema kuwa ni wakati wa kuacha kuwa wabobezi wa kujibu hoja na badala yake kuwa viongozi wa kuzuia hoja mapema.

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mkoa wa Singida, Bw. Othman Mwinjuma Jumbe, alisema kuwa lengo la mkaguzi si kuadhibu bali kuimarisha mifumo ya usimamizi wa fedha na utawala bora huku akisitiza kuwa Halmashauri zinapaswa kutumia taarifa ya ukaguzi kama kioo cha kuonyesha maeneo ya kuboresha na kuhakikisha mikopo inayotolewa inarejeshwa ipasavyo kwa ajili ya ustawi wa wananchi wote.

Vikao hivyo vya Itigi na Manyoni vimeweka msingi wa mwelekeo mpya wa uwajibikaji, nidhamu, na mabadiliko ya kiutendaji katika usimamizi wa fedha za umma, vikiwa ni kielelezo cha dhamira ya Mkoa wa Singida kuhakikisha maendeleo yanatokana na uwazi, weledi, na usimamizi makini wa rasilimali za wananchi.

Saturday, June 14, 2025

"VAENI VIATU VYA WANANCHI KATIKA MAAMUZI YENU" – RC HALIMA DENDEGO


Posted on: June 14th, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amewataka madiwani pamoja na watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida na Halmashauri ya Manispaa ya Singida kuhakikisha kuwa katika kila maamuzi wanayofanya wanajikita katika maslahi ya wananchi kwa kuwawakilisha kwa uaminifu na uadilifu mkubwa.

 Ametoa rai hiyo wakati wa vikao maalum vya mabaraza ya madiwani kwa ajili ya kupokea taarifa za utekelezaji wa mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). Amesema maamuzi yote yanapaswa kufanyika kwa kutanguliza dhamira njema kwa wananchi. “Katika siku zote unapofanya kazi, maamuzi utakayofanya, namna unavyofanya ile kazi, vaa kwenye viatu vyako, pima lile joto, ukiona kwamba linakubariki endelea kufanya, ukiona hata wewe unapata ukakasi, achana na mambo haya,” amesema RC Dendego.

Katika kikao cha Halmashauri ya Wilaya ya Singida, RC Dendego ameagiza watumishi wa halmashauri hiyo wanaodaiwa zaidi ya Shilingi milioni 6 walizokusanya kutoka vyanzo mbalimbali vya mapato lakini hawakuzifikisha benki, kuhakikisha wanazirejesha ndani ya siku saba. “Afisa Utumishi hao watumishi wanaodaiwa hizo fedha si wapo? Hatuna sababu ya kuendelea na hoja ya Shilingi milioni 6, ni kuichafua halmashauri, naagiza ndani ya siku saba watafute hizo fedha popote, ikigonga ile siku ya saba unakuja kunieleza kwa maandishi wameshalipa,” amesisitiza.

Kadhalika Amepongeza pia juhudi za madiwani katika kupigania maslahi ya wananchi na kuwataka waendelee na moyo huo huo kwa kuwa hoja zinazojadiliwa zinaathiri maisha ya kila siku ya mwananchi wa kawaida.

Katika Manispaa ya Singida, RC Dendego amesisitiza umuhimu wa ukusanyaji wa mapato kwa asilimia 100 na kuonya kuwa wakuu wa idara ambao hawafanyi kazi kikamilifu watahamishiwa vijijini. “Kukaa mjini ni fursa, na kama hufanyi kazi tutakupeleka kijijini,” amesema. Pia ameagiza Katibu Tawala wa Mkoa kuitisha mkutano wa dharura na kamati ya mikopo ya wanawake, vijana na walemavu kwa ajili ya kubaini changamoto zilizopo na kuzitatua haraka. “Tusikae kiboss, tukae kama wahudumu,” ameongeza.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amepongeza juhudi za halmashauri hizo kwa namna wanavyoshughulikia hoja za CAG kwa weledi na bidii. Ameeleza kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Singida imeonekana kuwa na idadi ndogo ya hoja ikilinganishwa na halmashauri nyingine mkoani humo, jambo linaloashiria ufanisi wa watendaji wake.

 Katika Manispaa,  Daktari Mganga amehamasisha matumizi ya fursa zilizopo kwa ajili ya kuongeza mapato na kupendekeza kuanzishwa kwa SPV (Special Purpose Vehicle) ya kusimamia miradi ya maendeleo ya kimkakati mjini Singida.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Mhe. Elia Digha, amesema kuwa tangu aingie madarakani hoja zilipungua kutoka 150 hadi 27, ambapo 19 zimefungwa na 8 ziko katika hatua ya mwisho. Amesema hoja za zamani zilikuwa 17 na hadi sasa 10 zimefungwa na 7 zimebaki. 

Ameeleza kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya kazi ya pamoja ya viongozi na watendaji, na kuwataka waendelee kushirikiana hata katika kipindi cha uchaguzi mkuu kinachokuja, akisisitiza kuwa huduma kwa wananchi haina msimu.

Kwa upande wa Manispaa, Meya wa Singida, Mhe. Yagi Maulidi Kiaratu, amewataka madiwani kutafuta suluhisho la hoja zilizobaki kwa lengo la kuiwezesha halmashauri hiyo kuondokana na changamoto za ukaguzi na kuongeza uwajibikaji.

 Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida, Bi. Joanfaith Kataraia, amesema kuwa Manispaa hiyo imepokea hati safi kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Amesema hoja 64 zilijadiliwa, 47 zikafungwa, 5 ni za kisera na 12 ziko kwenye hatua za utekelezaji. Halmashauri inaendelea na zoezi la kufunga hoja hizo kwa ukamilifu.

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Mkoa wa Singida, Bw. Othman Mwinjuma Jumbe, amepongeza juhudi za halmashauri zote mbili na kuhimiza kuendelea kupunguza hoja kwa kufuata mapendekezo ya ukaguzi na kutumia vyema fedha za serikali. Amesisitiza kuwa fedha zisipotumika kwa mujibu wa sheria, hurudi Hazina Kuu, hivyo ni muhimu watendaji kufanya kazi kwa bidii ili fedha za maendeleo ziwafikie wananchi.

Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, amesema kuwa wamejipanga kufanikisha makusanyo ya mapato kwa asilimia 100 kama alivyoelekeza Mkuu wa Mkoa. Amepongeza pia wanasheria wa halmashauri kwa kazi nzuri ya kushughulikia kesi mbalimbali za halmashauri, akibainisha kuwa usimamizi wa fedha za umma ni jukumu la kila mmoja.

Kwa ujumla, mikutano hiyo ya mabaraza ya madiwani imeonesha dhamira ya dhati ya viongozi wa Mkoa wa Singida katika kuhakikisha uwajibikaji, usimamizi thabiti wa fedha za umma, na ufanisi wa utendaji kazi ndani ya halmashauri kwa lengo la kuwaletea maendeleo wananchi wa Singida.

Wednesday, June 11, 2025

WANANCHI WA SINGIDA WALETEWA "UGALI MEZANI"


Posted on: June 11th, 2025

Mkoa wa Singida unatarajiwa kuanza kunufaika na rasilimali zake adhimu ikiwemo madini yanayopatikana katika hifadhi  na mapori tengefu yaliyopo mkoani hapa.

Hayo yamethibitishwa na Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego wakati wa ukaguzi wa miradi ya maendeleo inayofanywa na Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Singida Wilayani Manyoni kama moja ya kufatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama Tawala.

Mhe.Dendego amesema kwamba kuna taarifa za uwepo wa madini katika mapori ya akiba ya Rungwa,Kizigo na Muhesi ambapo inadaiwa kuwanufaisha watu wachache ambao wamevamia maeneo hayo na kufanya shughuli za uchimbaji madini bila kibali maalumu.

"Maeneo hayo yamekua na madini na vijana wanavamia pasipo mpangilio hivyo tufanye utafiti kubaini maeneo hayo Ili tuombe kibali kwa Mamlaka husika wananchi wetu na vijana wetu waweze kupata leseni Ili wachimbe kwa kufata utaratibu na hii itakuza mapato kwa wananchi wetu lakini pia kwa Halmashauri husika"

Kutokana na hilo ameunda kamati ya wajumbe maalum ya kufanya utafiti wa kina juu ya uwepo wa madini hayo katika mapori hayo sambamba na kutambua mipaka ya eneo hilo.Kamati hiyo inajumuisha Wakuu wa Wilaya ya Manyoni na Iramba,Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni,Afisa Viwanda na Biashara Mkoa wa Singida na wengineo.

Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Singida,Mhe.Martha Mlata akizungumzia suala hilo amesema kuwa Mkoa wa Singida unakwenda kupata neema kubwa ya maendeleo ya kasi kutokana na uwepo wa kibali na leseni ya umiliki wa maeneo hayo adhimu yenye madini hayo kwani baada ya kupata kibali hicho Taasisi,Halmashauri,watu binafsi na wananchi wa Singida kwa ujumla watapata nafasi ya kumiliki vitalu vya uchimbaji madini hivyo kukuza vipato vyao.

Kadhalika ameshauri leseni zilizopo kwa sasa zifutwe kwanza baada ya utafiti ili wanufaika wa kwanza wa madini hayo wawe wananchi wa Singida na Halmashauri zake ambapo zitapewa leseni ya kuajiri wachimbaji wadogo na kuwezesha Halmashauri kukuza mapato sambamba na ajira kwa wachimbaji wadogo.

Awali,Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Dendego amethibitisha kuwa Mhifadhi na Waziri wa Maliasili ma Utalii wameridhia ufanyike utaratibu wa kutambua maeneo hayo yenye madini ili kuombewa kibali ambazo zitawezesha utolewaji wa leseni zitakazowawezesha wachimbaji kufanya shughuli zao.

Upatikanaji wa madini katika maeneo hayo Mkoani Singida unatarajiwa kuwa chachu kubwa ya maendeleo kwani uchumi utakua kwa kasi sambamba na maendeleo ya miji kwani barabara nzuri,sehemu za kulala wageni,hoteli za kisasa ni baadhi ya mabadiliko chanya yanayotarajiwa kutokea.Pia Mkoa wa Singida umebarikiwa kwa madini meupe "gypsum"yanayopatikana maeneo tofauti ikiwemo Halmashauri ya Itigi na Manyoni.