Friday, April 25, 2025

KUELEKEA MEIMOSI,RC DENDEGO ATANGAZA FURSA ZA UWEKEZAJI

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego amewakaribisha wawekezaji katika mkoa wa Singida kwa kuwahakikishia kuwa Singida ni salama na mahali rafiki kwa uwekezaji wa aina zote.

Ameyazungumza hayo leo Aprili 25,2025 katika mkutano na waandishi wa habari akiwakaribisha wageni na viongozi wote kushiriki sherehe Za Mei mosi Mkoani Singida huku akitaja fursa nyingi za biashara na uwekezaji zinazopatikana mkoani hapa .

Amesema kuwa Mkoa wa Singida una fursa adhimu ikiwemo watu wakarimu,rasilimali watu ya kutosha ikijumuisha idadi kubwa ya wasomi,ardhi nzuri ya mazao kukua vema kama vile alizeti,mpunga,dengu,korosho na mengine mengi.Pia kuna madini ya dhahabu ambayo yanapatikana katika mgodi wa Shanta ambao hivi karibuni utazinduliwa mgodi mwingine , 

Pia Mhe Dendego amesema Singida ni rafiki kwa uwekezaji kwani inafikika kwa urahisi sana kutokana na kuwa katikati ya nchi na miundombinu yake ya bara bara kuwa rafiki.

Ufugaji Mkoani Singda ni fursa kwa sababu ni rahisi kunenepesha mifugo mbalimbali na kusafirisha nyama nje ya mkoa sambamba na Ufugaji wa samaki katika mabwawa ambayo ni rafiki kutokana na uwepo wa maji baridi na salama kwa ufugaji samaki.

"Mkoani Singida tuna Upepo ambao unaweza kuzalisha umeme wa kutosha,pia uwepo wa vichaka adimu duniani vilivyopo Wilaya ya Manyoni ambayo mwekezaji atavuna hewa ya ukaa.Sambamba na hilo nawakaribisha wageni na wawekezaji wote kuchangamkia fursa ya nishati safi za kupikia kwani idadi ya kaya zinazohitaji nishati hiyo Mkoani hapa ni takribani kaya laki nne,hivyo ni fursa kwenu kuja kuwekeza katika kuuza vifaa mbali mbali vinavyohitajika katika majiko ya nishati safi pamoja na ubadilishaji wa mitungi."amesema Mhe.Dendego.

Mkuu wa Mkoa wa Singida ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wageni wote waliofika mkoani hapa kwa ajili ya mei mosi katika hafla ya utalii wa ndani ambayo watapata nafasi ya kuujua mkoa wa Singida vizuri zaidi,ambayo itafanyika Aprili 27,2025 ambapo watapata fursa ya kutembelea Shemu mbali mbali za kiutamaduni na kupata kuifahamu vema historia ya Mkoa wa Singida,mila na tamaduni na makabila yake .

Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Daktari Fatuma Mganga amewakaribisha wananchi wote wa Mkoa wa Singida kushiriki katika siku ya Mei Mosi kwa lengo kubwa la kumpokea na kumpa pongezi za dhati Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya muungano wa Tanzania kutokana na mambo mengi aliyoyafanya katika miradi ya maendeleo na ya kimkakati iliyofanyika Singida ikiwemo sekta ya afya na lishe,elimu, miundombinu na usafirishaji, michezo,maji,biashara na uchumi na mengine mengi ambayo yamekuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla na kurahisisha ubora wa maisha ya wananchi.

Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Amoni Kakwale amewatoa hofu wageni na wananchi wa Mkoa wa kwa kuwahakikishia usalama wao na mali zao kwa muda wote watakaokuwa mkoani Singida kusherehekea Meimosi huku akitoa rai kwa wale wote waliokuaudia kuitumia vibaya Meimosi ili kufanya uhalifu kwani itawapelekea kuchukuliwa hatua kali za kiusalama

Pia ametoa angaluzo kwa madereva wote hususan madereva wa magari ya serikali kuhakikisha wanafuata sheria zote za barabarani wakati wanapoendesha vyombo hivyo vya moto ili kuhakikisha usalama wao na wa watu wengine wanaotumia barabara.

Sambamba na maandalizi hayo,Mei Mosi Mkoani Singida linatarajiwa kuwa na usiku wa Kuku ( kuku festival), mashindano ya magari, ngoma za asili, makongamano na bonanza la wafanyakazi ilisindikizwa na kauli mbiu ya Mei mosi 2025

 "UCHAGUZI MKUU 2025,UTULETEE VIONGOZI WANAOJALI HAKI NA MASLAHI YA WAFANYAKAZI".

Wednesday, April 23, 2025

MADAKTARI BINGWA WABISHA HODI SINGIDA.

 


Madaktari Bingwa wa wajulikanao kama “Madaktari bingwa wa Dkt.Samia" wanatarajia kutoa huduma za kibingwa na bobezi kwa wananchi wa Mkoa wa Singida mwezi ujao(Mei).

Mkuu wa mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego amezungumza hayo katika mkutano na waandishi wa habari leo Aprili 23,2025 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa,amesema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali kusogeza upatikanaji wa matibabu katika maeneo ya vijijini

Amesema kwa awamu ya kwanza huduma hiyo inatarajia kuanza kutolewa tarehe 28.04 hadi 03.2025 na kuwataka wananchi kujitokeza kwenye hospitali ziliopo katika halmashauri zao.

Pia,Amesema kutakuwa na madaktari na wauguzi bingwa 49 wa magonjwa ya watoto, magonjwa ya uzazi na wanawake, upasuaji wa jumla, huduma ya usingizi na ganzi, Magonjwa ya pua koo na masikio,huduma za kinywa na meno na huduma za uuguzi na kinga.

Dendego Amefafanua kuwa katika awamu ya pili kutakuwa na huduma itakayoanza tarehe 05 hadi 09,2025 ambapo madaktari 55 watatoa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi katika hosptali ya rufaa ya mkoa wa Singida.

Hatua hiyo ikilenga kuwatibu wagonjwa waliopewa rufaa katika awamu ya kwanza katika halmashauri mbalimbali mkoani Singida.

“Kutakuwa na madaktari bingwa na bobezi 55 katika fani 16 zinazogusa magonjwa ya ndani, wanawake na uzazi,watoto, upasuaji, upasuaji wa mifupa,njia ya mkojo,macho, masikio pua na koo,urekebishaji wa kinywa na meno, radiologia, usingizi na ganzi,urekebishaji wa kinywa na meno,utengemeo na viungo, mishipa ya fahamu na ubongo,ubingwa na ngozi, afya ya akili,na urekebishaji wa viungo;”alisema Dendego.

Aidha amewataka wananchi wenye magonjwa yaliyotajwa wajitokeze katika hosptali iliyopo kwenye Halmashauri zao ili kukutana na madaktari kwa kusikilizwa na kupatiwa tiba.

“Niseme wananchi wote mhakikishe mnafika mapema mtakuta timu hizo zimejipanga ili ziweze kuwashugulikia ,” Amesema Mhe.Dendego

Pia Amesema mkoa wa Singida unaendelea kumshukuru Rais Dr Samia Suluhu Hasan kwa kusogeza huduma karibu na kuwaepushia wagonjwa kwenda mbali kutafuta matibabu

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa,Dkt.Victorina Ludovick amesema kwenye Hospitali ya rufaa ya Mkoa wanatarajia kuwafikia watu takribani elfu tatu na huku kila Halmashauri wakitarajia kufikia zaidi ya watu elfu nne.


VIDEO:



Tuesday, April 22, 2025

MASHINDANO YA MICHEZO MEIMOSI SINGIDA YAZINDULIWA.


"Michezo ni Afya"

Haya yamesemwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Patrobas Katambi wakati akizindua Mashindano ya Michezo mbalimbali kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Meimosi Kitaifa Leo tarehe 22 Aprili 2025 katika viwanja vya CCM Liti Mkoani Singida, Mashindano haya yalianza tarehe 16 Aprili na yatahitimishwa tarehe 30 Aprili.

" Michezo ni muhimu sana katika maisha yetu ili kujenga afya zetu lakini pia michezo inatufanya tuchangamke katika kufanya maamuzi na ni sehemu nzuri yetu wafanyakazi kujenga urafiki na kufahamiana"

Aidha, Katambi amesema serikali imetoa Fedha nyingi kuwekeza kwenye michezo kwasababu inaelewa na kutambua umuhimu wa michezo katika maisha yetu.


"Mhe. Rais ametoa Fedha nyingi kujenga viwanja kwenye mikoa mbalimbali ndani ya nchi yetu ikiwemo Arusha lakini pia uwanja wetu wa Mkapa umekarabatiwa vizuri kwasasa hiyo yote ni kuonesha umuhimu wa michezo hivyo tumuunge mkono Mama yetu ili tufike mbali"

Akizungumzia suala la Ushiriki wa Taasisi katika Mashindano haya kuelekea Maadhimisho ya Meimosi Naibu Waziri Katambi amefafanua kuwa Taasisi 44 zimeleta washiriki lakini zingine hazijaleta washiriki hii ni wazi kuwa hawaungi mkono juhudi za Mhe. Rais kwenye suala la Michezo na ikumbukwe kuwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ndio Muajiri namba Moja hivyo Wakuu wa Taasisi tujitahidi kuhakikisha tunaleta watumishi kushiriki Michezo hii"

  Amebainisha kuwa Siku ya wafanyakazi Kitaifa ambayo itafanyika tarehe 01 Mei katika Mkoa wa Singida Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan ndiye Mgeni Rasmi.





               *KARIBU SINGIDA MEI MOSI 2025*






Sunday, April 13, 2025

SINGIDA YAPAMBANA NA WIMBI LA WATOTO WA MTAANI – SERIKALI YATOA MWELEKEO MPYA WA MALEZI

 



Singida, Aprili 12, 2025 

 Serikali ya Mkoa wa Singida imetangaza msimamo mpya kuhusu udhibiti wa ongezeko la watoto wa mtaani, ikisisitiza ushirikiano wa familia, viongozi wa dini, jamii na taasisi za serikali katika kuimarisha malezi na kusaidia watoto waliotengwa kurejea kwenye mazingira salama.

Akizungumza katika Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Mtaani yaliyofanyika katika Ukumbi wa Social jijini Singida, Katibu Tawala wa Mkoa, Dkt. Fatuma Mganga, alisema kuwa mkoa umejipanga kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa familia au huduma muhimu kwa sababu ya migogoro ya kifamilia, mmomonyoko wa maadili, au uzazi usio na uwajibikaji.

"Malezi bora siyo kumpendeleza mtoto tu—wakati mwingine lazima achapwe ili akue. Lakini pia watoto wajue kuwa kufundishwa na kusahihishwa si mateso. Mitaani hakuna mzazi, hakuna usalama, na hakuna upendo wa kweli," alieleza Dkt. Mganga.

Alisisitiza kuwa wanaume wanapaswa kuwajibika katika malezi na kuacha tabia ya kukwepa majukumu baada ya mimba, jambo linalosababisha ongezeko la watoto wa mtaani.


"Hali ya maambukizi ya VVU kwa wasichana wadogo ni ya kutisha, na chanzo kikubwa ni wanaume wazima kuwarubuni watoto wa kike. Tukatae tamaa hizi na tuwalinde watoto wetu wote—wa kike na wa kiume," alisema Dkt. Mganga.

Afisa Ustawi wa Mkoa wa Singida, Bw. Edward Maselo, alisema kuwa takribani watoto 150 waliathirika kutokana na migogoro ya kifamilia, hasa kuvunjika kwa ndoa, jambo lililosababisha baadhi yao kukimbia familia na kuishi mitaani.

“Tumeendelea kuwafuatilia watoto hawa na kuwapatia huduma muhimu kama chakula, mavazi, elimu, na afya. Pia tunawaelimisha wazazi kuhusu malezi bora, huku tukitayarisha kampeni maalum za kuelimisha jamii juu ya haki za mtoto,” alieleza Bw. Maselo.

Afisa Ustawi wa Manispaa ya Singida, Bi. Dorah Simon, alifafanua kuwa maadhimisho hayo yamelenga kuongeza uelewa kwa jamii kuhusu changamoto zinazowakumba watoto wa mtaani na umuhimu wa jamii kuwatambua kama sehemu ya familia kubwa ya taifa.

“Watoto hawa wana haki ya elimu, afya, ulinzi na malezi kama watoto wengine. Jamii iwakumbatie na iwasaidie kurudi kwenye maisha ya kawaida,” alisema Bi. Dorah.

Katika tukio hilo, watoto waliowahi kuishi mitaani walitoa ushuhuda kuhusu maisha yao kabla na baada ya kupatiwa huduma na msaada wa kijamii. Pia, viongozi wa dini walihamasishwa kushiriki kikamilifu katika kuwaelekeza watoto katika maadili mema, hususan watoto wa kiume ambao wameripotiwa kuwa wachache katika nyumba za ibada.

Maadhimisho hayo yalifanyika kwa mafanikio makubwa na kuhitimishwa kwa wito wa ushirikiano kutoka kwa wadau wote wa jamii kuhakikisha watoto wa mtaani wanapewa fursa ya pili ya maisha bora.










RC SINGIDA ATOA MAELEKEZO YA KUBORESHA MIUNDOMBINU YA ELIMU KATA YA MSANGE,




Msange, Singida – Aprili 10, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ameendelea na ziara yake ya kikazi kwa kukagua maendeleo ya sekta ya elimu katika Kata ya Msange, Wilaya ya Singida, ambapo ametembelea Shule ya Sekondari Msange na kutoa maelekezo mahsusi ya kuboresha miundombinu ya shule hiyo.


Katika ziara hiyo, Mhe. Dendego aliipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Singida kwa juhudi zinazofanyika katika kuinua kiwango cha elimu, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza kasi na ubora katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa madarasa, mabweni na vyoo ili kupunguza msongamano wa wanafunzi na kuweka mazingira bora ya kujifunzia na kufundishia.


"Nimefurahishwa na kazi mnayoifanya, lakini tunahitaji kuongeza kasi na kuhakikisha miradi ya elimu inatekelezwa kwa viwango vya ubora vinavyotakiwa. Mazingira rafiki ya shule ni msingi muhimu wa kuinua ufaulu wa wanafunzi wetu," alisema Mhe. Dendego.

Aidha, alisisitiza ushirikiano wa karibu kati ya viongozi wa halmashauri, wazazi na jamii katika kusimamia miradi ya elimu, akihimiza matumizi ya rasilimali zinazopatikana ndani ya jamii ili kuharakisha maendeleo ya shule.

Mhe. Dendego aliambatana na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, Mkurugenzi wa Halmashauri, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya pamoja na maafisa kutoka Ofisi ya Elimu Mkoa na Wilaya, katika kuhakikisha hatua za kimaendeleo zinatekelezwa kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, aliishukuru Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwa kuendelea kushirikiana bega kwa bega na wilaya hiyo katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Aliahidi kusimamia kwa ukamilifu maagizo yote yaliyotolewa ili kuwaletea wananchi maendeleo yanayoonekana.

Ziara hii ni sehemu ya mkakati wa Serikali ya Mkoa wa Singida wa kufuatilia na kuhimiza maendeleo katika sekta ya elimu, sambamba na dhamira ya Serikali ya awamu ya sita ya kutoa elimu bora, jumuishi na yenye usawa kwa watoto wote wa Kitanzania.


















Friday, April 11, 2025

RC DENDEGO AWAPONGEZA REA KUFIKISHA UMEME VIJIJINI

 

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego amepongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kazi kubwa ya kufikisha umeme vijijini hali iliyobadili maisha ya wananchi vijijini.

Mhe. Dendego ametoa pongezi hizo Aprili 11, mkoani Singida wakati akifungua Mkutano wa Kwanza wa Mwaka kati ya Wabia wa Maendeleo katika Sekta ya Nishati (EDPG) pamoja na REA uliolenga kupitia bajeti na mpango kazi wa Wakala huo kwa mwaka 2025/26.


“Nishati ya umeme ni nguzo kubwa kwa maendeleo ya Taifa lolote na watu wake. Nishati ya umeme vijijini ni msingi mkuu wa kuimarisha maendeleo ya haraka katika vijijini vyetu. Sote tumeshuhudia matokeo makubwa kwenye ukuaji wa uchumi, kuboresha maisha ya jamii zetu pamoja na kuchagiza utoaji wa huduma za kijamii".

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Khatib Kazungu amewashukuru Wabia hao wa Maendeleo na kusema kuwa wamekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya sekta ya nishati nchini huku akiwahakikishikia kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nao kuhakikisha lengo la kuwafikishia nishati bora kwa bei nafuu wananchi wote linafikiwa.


Awali akizungumza, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meje Jenerali (mstaafu), Jacob Kingu amesema kuwa, Tanzania imepiga hatua kubwa katika usambazaji wa umeme vijijini na mafanikio hayo yametokana na dhamira ya Serikali pamoja na mchango wa Wabia wa Maendeleo na kuahidi kuwa, REB itaendelea kuisimamia Mejimenti ya REA kuhakikisha miradi yote iliyopangwa inafanikiwa kwa wakati na katika ubora uliokusudiwa.











         *KARIBU SINGIDA:MEI MOSI 2025*